Kupanda na kushuka kwa Air
Tanzania
12/12/2008

Pichani ni moja ya ndege za Shirika la
Ndege Tanzania ambalo sasa huduma zake zimesimamishwa. SHIRIKA la Ndege
la Tanzania (ATCL), ambalo limekuwa na matatizo makubwa tangu ndoa yake
ya Shirika la Ndege la Afrika Kusini (SAA) ivunjike, limenyang’anywa
cheti cha kuruka angani na Mamlaka ya Anga (TCAA) baada ya kukosa
viwango vya ubora kuruka angani.
Taarifa kutoka ndani ya ATCL zimeeleza
kuwa shirika hilo limenyang’anywa cheti hicho tangu Disemba 8 mwaka huu
na hivyo litashindwa kusafirisha abiria hadi hapo litakapokidhi masharti
ya usalama wa anga ndipo itakaporejeshewa cheti hicho. Miongoni mwa
viwango hivyo vya usalama ni ukaguzi wa mara kwa mara wa ndege zake,
kuwa na wataalamu wa kutosha kama marubani na wahandisi, vitu ambavyo
vimeonekana kukosekana kwenye shirika hilo la serikali.
Kufungiwa huko kumekuja huku kukiwa na
uwezekano wa shirika hilo kufungiwa na Chama cha Kimataifa cha Usafiri
wa Anga (IATA) kufanya safari zake baada ya kubaini zaidi ya makosa 500.
Mwishoni mwa wiki iliripotiwa kuwa ATCL ilikaguliwa mwezi Oktoba na
kubainika na makosa hayo ya usafiri wa anga, lakini ikashindwa
kuyarekebisha na ndipo IATA ilipoanza mchakato wa kutaka kuizuia kufanya
safari. “Ni kweli ATCL imenyang’anywa cheti cha viwango kwa kukosa ubora
wa kuruka angani hivyo haitafanya safari za nje wala ndani ya nchi,”
alisema mmoja wa watu wa ndani TCAA alipohojiwa.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, ndege za ATCL
zilizokuwa zikifanya safari zake ndani na nje ya nchi haitaweza kufanya
tena safari hizo na vigogo wa ATCL jana walikuwa na vikao na TCAA
kuzungumzia suala hilo. Alipoulizwa kuhusu suala hilo katibu mkuu wa
Wizara ya Miundombinu, Omar Chambo alisema hana taarifa kuhusu
kunyang’anywa cheti kwa ATCL na kudai kuwa mkurugenzi wa shirika hilo,
David Mataka ndiye anayeweza kueleza suala hilo. “Sina taarifa kuhusu
suala hilo... hayo ni mambo ya ATCL na anayeweza kukueleza ni Mataka,
hivyo wasiliana naye... haiwezekani toka tarehe nane hadi leo mimi sijui,”
alisema Chambo.

Kupozi au kuruka, ukweli utafichuka.
|