Uwekezaji wasisitizwa
Ughaibuni
03/07/2008

Balozi
Mh. Mwanaidi Maajar akimkaribisha Bw. Issa Omar atoe mada yake juu ya
ujasirimali.

Bw. Omar
akihutubia umati wa wajasiriamali waliofika kwenye mkutano huo.

Mwenyekiti wa jumjuiya ya Watanzania waishio Uingereza Mh. Abubakar
Faraj akitoa hotuba.

Baadhi ya Watanzania waliofika katika
mkutano huo.

Wajasirimali waliofika
katika
mkutano katika jengo la Ubalozi wa Tanzania, London, Uingereza (Tanzania
House), wakisikiliza jambo katika hotuba iliyotolewa ya kuwahimiza
Watanzania kuwekeza nyumbani, Tanzania.
Bw. Issa
aliainisha fursa nyingi za biashara zilizopo Tanzania baada ya Serikali
kufungua milango zaidi ya uwekezaji na kupatikana kwa wawekezaji wakubwa
wa Kimataifa.
Akifafanua zaidi mtaalam huyo alisema hivi sasa takwimu zinaonyesha kuwa
Tanzania inahitaji zaidi biashara za uwezo wa kati (medium enterprises)
ili kuziba pengo kubwa kati ya wafanyabiashara wakubwa na wadogo.
Alisema ili kuendelea zaidi kiuchumi, makampuni makubwa yanahitaji sana
makampuni ya kati kwa ajili ya kutengeneza mali ghafi, kuzalisha nguvu
kazi na kutoa ushauri wa kitaaluma.
Katika Mkutano huo ulihudhuriwa na Watanzania zaidi ya 30, Bw. Issa
aliwashauri wajasiriamali hao kubuni miradi mbalimbali itakayowawezesha
kupata mikopo kwenye benki za Tanzania ili kuweza kuanzisha biashara
huko nyumbani. Aliwapa changamoto kuangalia fursa za biashara za huduma
na ushauri wa kitaaluma.
Alisema benki nyingi hivi sasa nchini Tanzania zinawatafuta wenye miradi
ya uhakika ili kuwakopesha mitaji ya kufanya biashara nchini humo.
Alisema kwa elimu, upeo na uzoefu waliokuwa nao, wajasiriamali hao
wanaweza kuanzisha miradi mizuri itakayowezesha kuinua uchumi wa
Tanzania.
Kwa mafanikio zaidi, Bw. Issa amewashauri wajasiriamali hao kujiunga
katika vikundi ili kuweza kujumuisha utaalam na mitaji ya msingi ya
kuanzisha miradi hiyo. Alisema biashara nzuri inahitaji utafiti wa soko,
udhibiti na shauku ya maendeleo zaidi.
Katika maswali yao kwa mtoa mada, wajasiriamali hao walipenda kufahamu
mipango zaidi ya Serikali kuondoa urasimu. Bw. Issa aliwaambia kwamba
wakati Serikali inaendelea na hatua mbalimbali kurekebisha mazingira ya
uwekezaji na biashara nchini Tanzania, ni vyema Watanzania hao pia
kutimiza wajibu wao badala ya kukaa tu kusubiri Serikali kufanya kila
kitu. Alifafanua kwamba Watanzania walioko nje ya nchi wana uwezo mkubwa
sana wa kubadilisha mazingira ya uwekezaji kama watarudi nyumbani na
kuingiza utamaduni mpya wa kikazi.
Awali akimkaribisha mtoa mada, Balozi Mwanaidi Sinare Maajar alisema
kwamba Ubalozi hivi sasa unafanya jitihada za kuwaunganisha
wajasiriamali wa Kitanzania wa ngazi zote walioko Uingereza ili
kuwashirikisha kikamilifu na Baraza la Biashara la Tanzania (Tanzania
Business Council).
Bw. Issa yupo London kwa ajili ya Mkutano wa Uwekezaji wa Africa (Africa
Business Forum 2008) ulioandaliwa na Commonwealth Business Forum.
|