ONYO kutoka Baraza la
Sanaa la Taifa (BASATA)
04/06/2008

ONYO KUHUSU BAADHI YA BENDI KUWAONYESHA
WANENGUAJI NUSU UCHI KATIKA MAJUKWAA YA MUZIKI.
Hivi karibuni Baraza la sanaa la Taifa limeshtushwa na kasi ya
mmomonyoko wa maadili ya watanzania kwa baadhi ya bendi za muziki wa
dansi nchini kutumia majukwaa ya dansi kwa makusudi kudhalilisha
wanenguaji wa kike, kudhalilisha watazamaji na kuwaharibu watoto wadogo
kwa baadhi ya wanenguaji wakiwa na vichupi na wanenguaji kuonekana kuwa
nusu utupu.
Baadhi ya wamiliki wa bendi wameiga tabia ya baadhi ya wanamuziki wa
nchi jirani kwa kuonyesha wanenguaji nusu utupu.Tabia hiyo imechukuliwa
kama biashara katika kumbi za maonyesho ya muziki na mbaya zaidi ni
kwamba biashara hiyo haiishii hapo bali imewafikia watoto wadogo kwa
kuona dhambi hiyo kupitia vyombo vya habar.Hayo tumethibitisha katika
ukaguzi wa kushtukiza uliofanywa na watendaji wa Baraza kati ya tarehe
24/5/2008 hadi tarehe 1/6/2008.
BASATA linachukua fursa hii kuwaaasa wamiliki wa bendi zenye tabia hiyo
kuacha mara moja na ikithibitika kuendelea kuvunja agizo hili,bendi hizo
zitachukuliwa hatua ikiwa ni pamoja na kuzifungia kufanya maonyesho au
kuzifutia usajili.
Aidha tunawaomba wamiliki wa vyombo vya habari kuacha kuwaunga mkono
wadhalilishaji hawa kwa kutoonyesha au kuchapisha picha za wanenguaji
waliovaa vichupi ili kulinda maadili yetu ya kutoharibu kizazi chetu
ambacho hivi sasa kinaharibiwa kwa kuonyesha watoto mambo ambayo
hawastahili kuyaona katika umri walio nao.
Ni nafasi hii pia tunawaomba wanenguaji wakike kuacha kutumika kama
chombo katika biashara za watu kwa kudhalilishwa utu wa mwanamke.Aidha
BASATA linawaomba wanaharakati wa haki za binadamu,wanaharakati wa
masuala ya wanawakae kutokaa kimya katika suala hili,kwani maadili ya
watanzania yanapobomolewa umma wa watanzania ndio unaoteketea.
Pia wadau wa muziki tunawaomba zikatae bendi zinazoonyesha vichupi na
wasiositiri mwili wa mwanamke hadi watakapobadili tabia hizo,tukiweka
tafakari kuwa,watazamaji wangejisikiaje kama binti zao na dada zao
wangecheza na vichupi mbele yao.
Tunaamini kuwa biashara ya muziki itafana kwa kuwa ubora wa muziki
wenyewe unaoambatana na uzingatiaji wa maadili (mila desturi)na kamwe
vichupi havitaupamba muziki mbovu kuwa muziki bora.
Imetolewa na
D. Lauwo
KAIMU KATIBU MTENDAJI
BASATA
2 JUNI,2008
|