MAXIMO aongezewa mkataba
19/06/2008

Kocha wa timu ya taifa ‘Taifa Stars’
Marcio Maximo (Pichani) ameongezwa mkataba na Shirikisho la soka
Tanzania (TFF) baada ya kuridhika na kazi aliyoanza kuifanya ambayo
imeipandisha chati Tanzania katika medani ya soka.
Rais wa TFF, Leodegar Tenga alisema hayo jana jijini Dar mwezi mmoja
kabla ya kumalizika kwa mkataba wa kocha huyo wa miaka miwili. Mkataba
wa miaka miwili aliosaini kocha huyo kutoka Brazil utamalizika mapema
mwezi ujao.“ Maximo aliingia mkataba nasi wa miaka miwili kuanzia Julai
28, 2006 hivyo mkataba wake huo utakamilika Julai 2,mwaka huu hivyo
tumeona ni vema tulizungumzie jambo hili mapema na tumeamua kumwongezea
mkataba huo kwa miaka miwili mingine” alisema Tenga.

Hata hivyo Tenga alisema pamoja na TFF kuamua kumwongeza mkataba wa kwa
miaka miwili mingine na Kocha Maximo katika mazungumzo yao juu ya
kuongezwa mkataba huo ameomba uongezewe mwaka mmoja tu kutokana na
sababu zake binafsi ambazo hakuzitaja.
Akizungumza mara baada ya Tenga kutangaza uamuzi wa TFF kumwongezea
mkataba wa kuinoa Stars, Maximo alisema sababu kubwa ya kufurahia jambo
hilo na kushukuru kwa ushirikiano aliopewa kutekeleza majukumu yake na
kueleza kuwa sababu yake ya kuomba apewe mwaka mmoja tu katika mkataba
mpya ni kutoa nafasi kwa makocha wengine kuendeleza pale alipofikia
katika programu ya kuinua na kuendeleza soka la Tanzania.

“Unajua mtu huwezi kutekeleza programu ya miaka 10 ya kuinua na
kuendeleza soka la nchi pekee yako kwani kila programu ya kocha ina muda
wake wa kukamilika hivyo katika mikaka hiyo 10 kuna ulazima wa kocha
mwingine kuja kuendeleza pale nilipofikia” alisema Maximo.
Maximo aliiwezesha timu ya Taifa Stars
katika mechi ya juzi kutoka 0-0 na timu ya Cameroon katika kuitafuta
tiketi ya kwenda kushiriki kombe la dunia 2010 Afrika ya Kusini.
|