Wanne watiwa ndani kwa
janga la Disko Toto Tabora
14/10/2008

Jengo lililokuwa na ukumbi wa Disco la
Bubbles, uliosababisha maafa siku ya Eid ya kwanza ya Eid-el-fitr.
WATU
wengine wawili wamekamatwa wakituhumiwa kuhusika na tukio
lililosababisha vifo vya watoto 19 waliokufa wakati wanacheza muziki
siku ya Eid Mosi.
Polisi
imesema kuwa waliokamatwa ni Meneja wa disko la One Ten Teck, Jaffar
Rashid na Meneja wa Bubbles Night Club, Vituko Salala.
Kabla ya
kukamatwa kwa mameneja hao, Polisi waliwakamata wamiliki wa madisko hayo
ambao ni Projestus Fidelis na Shashikant Manji Patel.
Kwa
mujibu wa vyombo vya dola watu hao ndio waliandaa disko la watoto katika
siku hiyo ya Eid-el-fitr. Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Abeid Mwinyimsa,
alisema leo kuwa wakurugenzi hao na mameneja wanashikiliwa na polisi kwa
ajili ya kuhojiwa kuhusu chanzo cha tatizo lililosababisha watoto hao
kupoteza maisha.
Alisema
Polisi imempa taarifa rasmi ya kushikiliwa kwa watu hao, huku ikimuarifu
kwamba walinzi wa milangoni katika madisko hayo mawili "Mabaunsa" nao
wanasakwa ili waweze kuhojiwa kuhusu sakata hilo. Mkuu huyo wa Mkoa
alisema wakurugenzi hao, watahojiwa pia na Tume huru iliyoundwa kwa
ajili ya kuchunguza mkasa huo, ambayo alisema imeshaanza kazi yake na
kuwataka wananchi waipe ushirikiano ili iweze kupata taarifa za ukweli
zitakazofanyiwa kazi na serikali.
Katika
siku hiyo ya Eid, watoto 19 walikufa na wengine kulazwa hospitali ya
mkoa ya Kitete baada ya kukosa hewa katika kumbi za disko wakati wakiwa
katika sherehe ya Eid-el-fitr.
|