Mount Kilimanjaro

Beit El Ajaib
     

HomeNewsServicesEventsAbout UsContact Us

 
ProfileToolsGamesCommunity

NEWS

 
 

Wakimbizi wa Burundi kuomba uraia Tanzania

24/10/2008

Habari na Muandishi Maalum, Urambo, Tabora

FAMILIA 8,307 za wakimbizi wa Burundi wanaoishi katika kambi ya wakimbizi ya Ulyankulu, wilayani Urambo, Mkoani Tabora, wameomba uraia wa Tanzania, Rais Jakaya Mrisho Kikwete ameambiwa leo, Ijumaa, Oktoba 24, 2008.

Akiwasilishiwa taarifa ya utendaji wa Serikali katika Wilaya ya Urambo katika siku ya pili ya ziara yake ya siku nane katika Mkoa wa Tabora mjini Urambo, Rais Kikwete ameambiwa kuwa familia hizo zina jumla ya wakimbizi 40,886.

Taarifa hiyo imesema kuwa baada ya baadhi ya wakimbizi kukubali kurejea nyumbani kwao Burundi, kiasi kubwa cha wakimbizi wameomba uraia wa Tanzania baada ya kuwa wamekaa nchini kwa miaka mingi kama wakimbizi.

Baada ya kuwa amejulishwa habari hizo, Rais Kikwete amesema kuwa ni vyema kuachia mchakato wa kuomba uraia kuendelea kwa kushughulikiwa na taasisi husika, na kuwa baada ya kuwa umekamilika Serikali itachukua uamuzi kuhusu wapi wataishi wakimbizi hao.

Hata hivyo, amesema kuwa wakimbizi hao hawataruhusiwa kukaa katika eneo hilo la Ulyankulu, na badala yake watahamishiwa katika sehemu mbali mbali nchini.

“Tuachia mchakato uendelee wa kuwapa uraia wa Tanzania kama wanazo sifa za kupata uraia huo. Lakini lazima kusema kuwa wakishakuwa wamekubaliwa kuwa raia wa Tanzania watasambazwa nchi nzima, kwa sababu hawaombi kuwa raia wa Ulyankulu, bali raia wa Tanzania,” amesema Rais Kikwete.

Ameongeza: “Wajue na wajulishwe kuwa wanaomba kuwa raia wa Tanzania, na siyo kubakia Ulankulu. Vinginevyo, wakiendelea kubakia katika eneo la sasa la ukimbizi wataendelea kuwa wakimbizi. Lakini kwanza tuangalie maombi yao na kuyachambua vizuri.”

Akizungumzia suala la mauaji ya albino kwenye kikao hicho, baada ya kuwa amepongezwa na wilaya kwa msimamo wa Serikali yake kuhusu mauaji hayo, Rais amesema kuwa ni ujinga kudhani kuwa ukikata na kupata kidole cha albino basi utaweza kupata utajiri.

“Sasa kama utajiri si wangeupata albino wenyewe kwa sababu wao wanacho kila kitu, wanayo mikono, wanazo nywele, wanavyo vidole, sasa kwa nini kama viungo hivyo vinaleta utajiri wasiwe matajiri wakubwa wa nchi yetu,” ameuliza kwa mshangao Rais Kikwete.

“Ni lazima watu wanaotaka kuwa matajiri wajue kuwa utajiri ni matokeo ya kufanya kazi kwa bidii, kwa maarifa na kwa nidhamu na siyo kuchuna ngozi ama kukata na kukimbia na viungo vya albino,” amesema Rais Kikwete.

Rais pia ameonyesha mshangao wake kwa baadhi ya watu na taasisi zinazoilaumu Serikali kutokana na mauaji ya albino.

"Kuilaumu Serikali kwa ukatili huu siyo jawabu. Hakuna mtu wa Serikali anayewashauri wauaji hao wa albino kuwafukuza wenzetu hawa na kuwakata viungo vya miili yao.

La msingi ni kwa taasisi zote, watu binafsi na Serikali,kushirikiana katika kutafuta jawabu la ujinga huu.”

 

   
 

Custom Search

Go up

 

Quick Links

Watch Television
News Archive

© www.zenjydar.co.uk - Since 2007 | Web master | Site map | www.zenjydar.co.uk - Since 2007 ©