Mount Kilimanjaro

 

 

 

Your community website

Beit El Ajaib
     

HomeNewsServicesEventsAbout UsContact Us

ProfileToolsGamesCommunity

NEWS

 
 

Muwafaka wa Kenya

29/02/2008

Rais Mwai Kibaki (kushoto) na Kiongozi Mkuu wa chama cha Upinzani nchini Kenya cha
ODM Raila Odinga(kulia)wakitia saini baada ya kufikia muafaka ambao waziri mkuu wa kenya sasa atatoka chama kikuu cha upinzani nchini humo ambacho ni ODM kinachoongozwa na Raila Odinga, Muafaka huo umefikiwa chini ya Mpatanishi wa kimataifa na katibu mkuu mstaafu wa umoja wa mataifa Koffi Annan wa pili kushoto mstari wa nyuma, Rais Jakaya Kikwete wa kwanza mstari wa nyuma kushoto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Africa Union,na Rais Mstaafu wa Tanzania Benjamin Mkapa kwa kulia mstari wa nyuma.

HATIMAYE mahasimu wakubwa katika siasa za Kenya, Rais Mwai Kibaki na kiongozi wa Chama cha ODM, Raila Odinga, wamekubaliana kimsingi kuundwa kwa serikali ya mseto nchini humo.

Viongozi hao wawili walitia saini makubaliano hayo ambayo yanapewa nafasi kubwa ya kumaliza hali ya uhasama wa kisiasa nchini humo, uliodumu tangu kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi wa urais Desemba 30, mwaka jana.

Makubaliano hayo ambayo yamezipa ushindi pande zote mbili, ule wa Rais Kibaki na Odinga, yalifikiwa kutokana na jitihada za jumuiya ya kimataifa zilizokuwa zikiongozwa na Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa, Kofi Annan, aliyekuwa akisaidiwa na watu wengine wawili maarufu Afrika, Rais mstaafu Benjamin Mkapa na Graca Machel, ambaye ni mke wa Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela.

Aidha, kufikiwa kwa makubaliano hayo jana kulichangiwa pia na juhudi za Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika ( AU), Rais Jakaya Kikwete, ambaye tangu juzi alikuwa nchini Kenya kuyapa mazungumzo hayo msukumo.

Uamuzi wa Kikwete kwenda Kenya ulikuja siku ile ile Annan ambaye ndiye msuluhishi mkuu wa mgogoro huo alitangaza kusitisha kwa muda mazungumzo hayo kutokana na pande zinazohusika kusuasua kufikia maamuzi.

Aidha, kabla ya Kikwete kwenda Kenya, siku chache zilizopita alikuwa amepokea ujumbe maalumu kutoka kwa Rais Kibaki uliowasilishwa Ikulu Dar es Salaam na Makamu wa Rais wa Kenya, Kalonzo Musyoka.

Kwa upande mwingine, kufikiwa kwa makubaliano hayo, kumehitimisha machafuko ambayo yamegharimu maisha ya Wakenya wapatao 1,000 huku wengine zaidi ya 300,000 wakihangaika baada ya kupoteza makazi yao.

Akizungumza muda mfupi baada ya Kibaki na Odinga kutiliana saini makubaliano hayo, Annan alisema: “Yalikuwa muhimu ili kuinusuru nchi hii.”

Kwa mujibu wa makubaliano hayo, serikali ya mseto baina ya vyama hivyo itaundwa kwa kuangalia nguvu ya chama katika bunge la nchi hiyo.

Aidha, chini ya makubaliano hayo, chama chenye wabunge wengi ndicho kitakachounda serikali, hatua ambayo kwa namna yoyote ile inampa Raila nafasi kubwa ya kuchukua wadhifa huo mara tu baada ya Bunge kuridhia muafaka huo wa jana.

Akitangaza misingi mingine ya makubaliano hayo, Annan alisema waziri mkuu atakayeteuliwa atathibitishwa na bunge na yeye ndiye atakayekuwa mkuu wa shughuli za kila siku za serikali.

“Katika makubaliano hayo waziri mkuu mpya atakuwa na mamlaka ya kusimamia shughuli za serikali,” alisema Annan.

Mbali ya waziri mkuu, vyama viwili, kile cha PNU na ODM, kila kimoja kitatoa naibu waziri mkuu na hivyo kufanya wadhifa huo kushikwa na watu wawili.

Annan alisema mgawanyo wa nyadhifa katika serikali mpya ikiwa ni pamoja na ile ya waziri mkuu na manaibu wake wawili, utatokana na wingi wa wabunge wa kila chama ndani ya bunge.

Kutokana na makubaliano hayo, Annan aliwataka Wakenya kuunga mkono makubaliano hayo, akisema: "Kazi ya maridhiano na ujenzi wa taifa sio kwa viongozi pekee. Ni lazima ifanywe na kila upande, kijiji, na taifa zima.

"Ninatoa wito kwa Wakenya kuunga mkono hatua hii, ili Kenya iweze kurejea katika nafasi yake ya ushawishi wa kimaadili na injini ya uchumi wa Afrika. Na ningependa kuwahakikishia kuwa marafiki zenu wa Afrika na jamii ya kimataifa wako nyuma yenu."

Rais Kibaki alisema; "Hatua hii imetukumbusha kama taifa kuna mambo mengi yanayotuunganisha kuliko yanayotutenganisha.

"Tumekumbushwa kuwa ni lazima tufanye yote yaliyo katika uwezo wetu ili kulinda amani ambayo ndio msingi wa umoja wa taifa letu... Kenya ina nafasi kwa ajili yetu sote."

Kwa upande wake Odinga alisema: "Kwa kusaini makubaliano haya, tumefungua ukurasa mpya katika historia ya nchi yetu kutoka nyakati za mifarakano hadi za ushirikiano.

"Sisi kwa upande wetu tumejitoa kikamilifu kuhakikisha kuwa makubaliano haya yanafanikiwa," alisema.

Viongozi hao waliwashukuru watu wote waliokuwa pamoja na Wakenya katika kile ambacho Odinga alikiita "saa ya mahitaji ", akiwemo Annan, Umoja wa Afrika (AU), Umoja wa Ulaya (EU), Marekani na Umoja wa mataifa (UN).

Waliwataka Wakenya kuendelea mbele kwa pamoja bila kuruhusu migawanyiko kwa misingi ya kikabilia.

Akizungumza muda mfupi baada ya kuwasili Uwanja wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere jana jioni, Rais Kikwete alisema alipofika Kenya juzi alimkuta Annan ameshakata tamaa.

Kikwete aliwaeleza waandishi waliofurika uwanjani hapo kuwa, walipoangalia maeneo waliyokuwa wakitofautiana kina Kibaki na Raila.

Mimi sijui, nimeshiriki tu. Tumeangalia matatizo na kuyatambua lakini pia Wakenya walikuwa na matumaini kuwa sisi kwenda pale matatizo yao yangeisha. Matatizo hayo yameisha na wameridhika,” alisema Kikwete.

Alisema atawashangaa wanasiasa ambao watakwamisha makubaliano hayo ya jana ambayo waliyakubali wenyewe.

Alisema iwapo muafaka huo usingepatikana, Kenya isingetawalika tena, kwani hali ilikuwa ni ngumu na jana hiyo peke yake hadi kufikiwa kwa muafaka iliwachukua muda wa saa zipatazo tano kuafikiana.

Kwa mujibu wa Kikwete, kikubwa kilichokuwa kikiwatofautisha kilikuwa ni mamlaka atakayokuwa nayo waziri mkuu na haja ya mamlaka hayo kuingizwa katika katiba.

Rais Kikwete alieleza pia kuwa, katika mazungumzo hayo kulikuwa na hoja pia ya kurudiwa kwa uchaguzi na ile ya kuhesabiwa upya kwa kura milioni 11 mambo ambayo alisema kama yangefanyika yangechukua muda wa miezi mitatu na hivyo kusababisha machafuko.

Alisema hali hiyo ilisababisha masuala hayo yawekwe pembeni na kuweka mkazo katika kuangalia namna pande hizo mbili zitakavyoshirikiana.

Aidha, alisema matokeo ya mazungumzo hayo yamemfariji sana Rais Kibaki na akawapongeza Annan, Mkapa na Machel kwa namna walivyosimamia mazungumzo hayo magumu.

Wachambuzi wa siasa za Kenya wanasema kuwa kinachofuatia sasa baada ya makubaliano hayo ni pande hizo kuanza kusaka watu ambao watashika nyadhifa hizo mpya, huku nafasi muhimu na yenye mvutano zaidi ikionekana kuwa ile ya waziri wa fedha.

Hali hii imeifikisha Kenya hapo tangu ODM iliyokuwa imemsimamisha Odinga kugombea urais kugomea matokeo ya urais, ikisema yalikuwa yamempa Kibaki ushindi usiostahili.

Msimamo huo wa ODM kupinga matokeo ya uchaguzi wa urais, huku jumuiya ya kimataifa wakiwamo wasimamizi wa kimataifa wakiyatilia mashaka pia, uliibua vurugu kubwa na kusababisha taifa hilo ambalo limekuwa na amani tangu lipate uhuru wake mwaka 1963 kuingia katika mapigano ya kikabila.

 

   
 

Custom Search

Go up

 

Quick Links

Watch Television
Events Calendar
News Archive 2008
News Archive 2007

External Links

Alnoor CET
TZ Embassy UK
TZ's Community UK

© www.zenjydar.co.uk - Since 2007 | Web master | Site map | www.zenjydar.co.uk - Since 2007 ©