Buriani Mzee Shaaban
Khamis Mloo
15/03/2009

Muasisi wa chama cha CUF, Shaaban Khamis
Mloo, amefariki dunia jana asubuhi nyumbani kwake mjini Zanzibar.
Mazishi yake yalifanyika jana saa 10.00 alasiri huko huko Zanzibar.
Marehemu Mzee Mloo alikuwa katibu mkuu wa kwanza wa chama cha CUF kwa
miaka nane, kutoka 1992 hadi 2000 alipochukua nafasi ya umakamo
mwenyekiti hadi kustaafu kwake mwaka 2004.
Mzee Shaaban alikuwa miongoni mwa waasisi
wa Chama cha CUF kwa kuanzia na vuguvugu la KAMAHURU. Ni yeye ndiye
aliyeongoza mazungumzo ya kwanza na wakati huo aliyekuwa mwenyekiti wa
Chama hicho, James Mapalala, na hatimaye kuungana na kuzaliwa kwa CUF.
Chama hicho kinamtambua Mzee Mloo sio tu
kama kiongozi mstaafu wa Chama, bali zaidi kama muasisi au mwanzilishi
na alikuwa mwanachama imara na shupavu katika siku zote za uhai wake.
Atakumbukwa daima ndani na nje ya chama cha hicho kama mjuzi wa siasa za
Tanzania kwa ujumla, mchapakazi na mtu aliyekuwa na ujasiri wa kupigiwa
mfano.
Hata baada ya kustaafu umakamo mwenyekiti,
Mzee Mloo aliendelea kuwa sehemu muhimu ya CUF kwa kujitolea katika
mashauri mbali mbali. Kila alipokuwa na uwezo, hakuacha kuhudhuria
mikutano ya hadhara au vikao vyovyote ambavyo alialikwa.
Kikao cha mwisho kuhudhuria ni Mkutano
Mkuu wa Nne wa chama cha CUF uliofanyika katika ukumbi wa Diamond
Jubilee, Dar es Salaam, kuanzia 23 hadi 27 Februari, mwaka huu. Kwa
hivyo, hadi siku za mwisho mwisho wa uhai wake, Mzee Mloo alisimama
imara kuijenga na kuihuisha chama hicho cha CUF.
|