Tutatumia njia nyingine ya
kuzalisha umeme - Pinda
07/06/2009

WAZIRI MKUU Mizengo Pinda, amesema
Tanzania imelenga kutumia njia mbadala za kuzalisha umeme badala ya
kutegemea nguvu ya maji kama njia pekee ya kuzalisha nishati hiyo.
Alitoa kauli hiyo juzi alipokuwa
akizungumza na Mkurugenzi wa Uratibu wa Kanda wa Shirika la Umoja wa
Mataifa la Maendeleo ya Viwanda (UNIDO), Akmel Akpa alipokutana naye
nyumbani kwake Oysterbay, jijini Dar es Salaam.
Waziri Mkuu alisema pamoja na umeme
unaotokana na maji, serikali pia imeanza kutumia vyanzo vingine vya
kuzalishia nishati hiyo na kuvitaja vyanzo hivyo kuwa ni jua, upepo,
mawimbi ya bahari, gesi asilia na nishati mbadala inayozalishwa kwa
kutumia takataka na mimea.
“Mimi sikujua kama mawimbi ya bahari
yanaweza kuzalisha umeme na nilihofia usalama wa mitambo kwa sababu ya
chumvi nyingi kwenye maji ya bahari, lakini wataalamu wamenihakikishia
kuwa ni jambo linalowezekana kufanyika bila matatizo makubwa,” alisema.
Alisema inasikitisha kuona watu wa maeneo
ya vijijini wakikosa huduma za umeme na kuwafanya wategemee mno mafuta
ya taa ambayo ni ghali mno na kuni kama vyanzo vya nishati.
Alisema matumizi ya kuni, yamekuwa
yakichangia mno kuharibu mazingira na moshi unawaumiza macho wazee ambao
pia huishia kuitwa wachawi.
“Tumeanzisha Mamlaka ya Usambazaji Umeme
Vijijini (REA) kwa sababu tumepania kuinua hali za maisha katika maeneo
ya vijijini kwa sababu huko ndiko kutakuwa na uzalishaji mkubwa
kulingana na malengo ambayo serikali ya awamu ya nne imejiwekea na hasa
hili la kuinua kilimo,” alisema.
Alisema ili kuharakisha utekelezaji wa
mpango huo, serikali ilipitisha sheria ya umeme vijijini, ili watu
mbalimbali kutoka sekta binafsi ambao watakuwa na uwezo wa kuzalisha
nishati hiyo waruhusiwe kufanya hivyo.
Aliipongeza UNIDO kwa kusimamia miradi ya
uzalishaji nishati ya gesi asilia katika kiwanda cha kusokota mkonge cha
Katani kilichopo Hale, mkoani Tanga, ambacho kinazalisha kilowati 150
kwa kutumia makapi ya mkonge.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa UNIDO
alimweleza waziri mkuu juu ya kuwepo kwa haja ya bara la Afrika kujikita
katika uzalishaji wa nishati ili liweze kujihakikishia kuwepo kwa huduma
hiyo muhimu kwa miaka 20 hadi 30 ijayo.
Alisema upatikanaji wa uhakika wa huduma
ya nishati utaliwezesha bara la Afrika kujikita katika biashara ya mazao
ya kilimo na usindikaji wa mazao, mambo ambayo alisema UNIDO imeamua
kuyasimamia kikamilifu.
“Tunapaswa kusukuma jambo hili kama ajenda
mpya kwa bara la Afrika. Uhakika wa nishati utatuhakikishia maendeleo ya
bara letu, tutakuwa na uhakika wa kuuza bidhaa zetu kwa sababu tutakuwa
tumeziongeza thamani kwa kuzisindika na pia itatupa uhakika wa kipato,”
alisema.
Alisema pia kuna haja ya kuwa na kauli
mbiu mpya ya ’fursa za utajirisho’ kama kauli mbadala ya 'mkakati wa
kupunguza umaskini' na kwamba zikiandaliwa fursa za kuwawezesha watu
kupata ajira na kuuza bidhaa zilizosindikwa ni lazima watu wataweza
kuondokana na umaskini.
|