Kikwete aonya Mafisadi
12/06/2009

Katika mtikisiko wa uchumi duniani,
Serikali imetangaza kutenga shilingi trilioni 1.7 za mpango wa kupunguza
mzigo kwa wananchi wake kutokana na hali ya msukosuko wa kiuchumi, Rais
Jakaya Kikwete ameonya kuwa yeyote atakayejaribu kujihusisha na ujanja
ujanja wa kutaka kujitwalia fedha hizo kwa manufaa binafsi
atashughulikiwa ipasavyo.
Rais ametoa onyo hilo wakati akizungumza
na wabunge, wazee na wananchi wa mkoa wa Dodoma kuhusu hali ya uchumi
nchini.
Amesema Serikali imepanga kutumia kiasi hicho cha shilingi trilioni 1.7
katika bajeti yake ya mwaka mpya wa fedha na hivyo ni lazima zitumike
kwa malengo yaliyowekwa na si vinginevyo.
Akizungumzia kuhusu sekta mbalimbali
zinazoguswa na mpango huo, Rais Kikwete amesema, Serikali italipa fidia
vyama vya ushirika na makampuni yaliyonunua mazao na kushindwa kuwalipa
wakulima.
"Hatutalipa madeni ya zamani... na nitumie fursa hii kuwaonya watu
wanaopanga mikakati ya kujichomeka kiujanja ujanja ili watafune fedha
kwa maslahi yao binafsi," akasema.
Amesema msukosuko huo wa uchumi ni wa muda
na hivyo changamoto zilizopo ni kutafakari jinsi ya kujinusuru na nini
kifanyike ili kubadili uelekeo.
"Ni imani yetu kuwa msukosuko huu ni wa muda tu kwa kuwa umeshawahi
kutokea miaka ya nyuma na ukapita kiasi kwamba uchumi wa dunia ukakua
zaidi," amesema.
Ili kukabiliana na hali hiyo mikakati
mbalimbali iliyowekwa na Serikali ni kulinda ajira katika sekta
mbalimbali na kuhakikisha upatikanaji wa chakula.
Kadhalika kulinda sekta ya uwekezaji na kulinda mahitaji muhimu ya
kijamii ikiwa ni pamoja na afya na elimu.
Hotuba hiyo ya Rais Kikwete aliyoitoa kwa
zaidi ya saa moja katika ukumbi wa Kilimani mjini Dodoma pia
ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali na vyama vya siasa.
|