Kibaki avunja ukimya
15/06/2009

BAADA ya kukaa kimya kwa muda mrefu tangu
mgogoro wa kisiwa cha Migingo kilichopo ndani ya ziwa Viktoria
kinachogombewa kati ya nchi yake na Uganda uanze kunguruma, Rais Mwai
Kibaki ameamua kuvunja ukimya huo na kutaka mazungumzo yanayohusu kisiwa
hicho kuitishwa mara moja.
Rais Kibaki alivunja ukimya huo mwishoni
mwa wiki wakati akiwahutubia waombolezaji katika kijiji cha Sichei
kilichopo eneo la Bungoma, kaskazini mwa nchi hiyo waliokuwa
wamehudhuria kwa ajili ya mazishi ya mama mzazi (Bi Esther Nekesa
aliyefariki wiki iliyopita akiwa na umri wa miaka 85) wa Makamu wa
Kwanza wa Rais, Bw. Michael Kijana Wamalwa.
Rais Kibaki alisema kwamba timu ya pamoja ya wachunguzi ndiyo
itakayosema ukweli kuhusu mipaka kati ya Kenya na Uganda na akaonya kuwa
ni bora waiache tume hiyo ifanye kazi yake bila kuingiliwa.
Mbali na kutaka mazungumzo hayo yakome, Kiongozi huyo wa Kenya
aliwakemea wabunge wa Bunge la nchi hiyo kuacha kuelekeza mashambulizi
dhidi ya raia wa Uganda pamoja na kiongozi mwenzake, Rais. Yoweri
Museveni,akisema kuwa mashambulizi hayo ni lazima yakome mara moja.
“Tumechoka kuona wabunge wakijiingiza kwenye malumbano kuhusu Migingo
utadhani hakuna mambo mengine muhimu yanayoiathiri nchi. Hali hii
imezidi na nitaka malumbano haya yakome mara moja,”alisema Rais Kibaki.
Akizungumzia kuhusu msuada uliopitishwa
hivi karibuni na wabunge wanaoipinga Uganda ambao unamtaka Rais Kibaki
kutumia nguvu za kijeshi kukikomboa kisiwa hicho chenye mvutano endapo
jitihada za kidiplomasia zitakwama, alisema kwamba jambo hilo haliko
katika mipango yake.
“Vita haitatupeleka kokote. Uganda na
Kenya ni majirani na wenye lengo moja la kuwa na siasa moja ya
shirikisho na wala sio siasa ya pesa nane,"alisema Rais Kibaki.
Alisema, kitu ambacho mataifa yote mawili yanakihitaji kwa sasa ni kila
mmoja kufanya mazungumzo na mwenzake na sio kupoteza wakati kuzungumzia
kuhusu nani mmiliki halali wa kisiwa cha Migingo.
Rais Kibaki alisema kwamba makubaliano waliyotiliana sahihi na Rais
Museveni mjini Arusha yanaonesha wazi jinsi gani walivyoamua kulitafutia
ufumbuzi suala hilo la Migingo na akaongeza kwamba hivi sasa fungu
linakusanywa ili kutengeneza njia ya kisasa ya reli inayoziunganisha
nchi hizo mbili.
“Inaniumiza sana kuona wabunge wanamdhalilisha kiongozi wa Waganda. Rais
Museveni ana ufahamu kuliko ninyi nahitaji msitishe udhalilishaji kama
huo,” alisema Rais Kibaki.
Alisema, njia nzuri ni kwa raia wa Kenya kuzungumza na raia wenzao wa
Uganda ili kutafuta njia mbadala ya kuinua uchumi.
|