Hitma kwa waliokufa ajali
ya meli Zanzibar
21/06/2009

Uongozi
wa kampuni ya meli ya Fatih Express umeandaa hitma ya kuwaombea watu
sita waliopoteza maisha katika ajali ya meli hiyo iliyotokea hivi
karibuni katika bandari ya Zanzibar.
Mkurugenzi wa Kampuni hiyo, Said Abdulrahman Juma alisema kuwa, hitma
hiyo itafanyika katika msikiti wa Ijumaa wa Malindi baada ya swala ya
Alasiri na itahudhuriwa na wananchi mbalimbali wakiwamo na masheikh
mbalimbali.
“Tumeamua kufanya hitma kwa ajili ya ndugu zetu, sisi tumeguswa sana na
maafa hayo, hivyo tunaomba wananchi wote wanaoweza kuhudhuria wafanye
hivyo ili tuwaombee wenzetu” alisema Juma.
Habari za ziada, idara za mamlaka ya
bandari zikishirikiana na timu ya waopoaji wa meli hiyo iliyozama katika
bandari ya Malindi, Zanzibar Mei 29, 2009, ilionywa na Nahodha wa meli
hiyo bwana Usi Ali Usi katika uopoaji huo kuwa jitihada za kuopoa meli
hiyo zisipofanywa kwa umakini, zinaweza kusababisha uchunguzi wa ajali
hiyo kutokwenda sawa.

Nahodha Usi Ali Usi alizungumza na
waandishi wa habari kwa mara yake ya kwanza tangu kutokea ajali hiyo
alisema, taarifa kuwa meli hiyo inamomonyoka kutokana na kuchakaa wakati
wa kuvutwa si wa kweli.
Alisema tatizo ni watu kutofunga minyororo
katika sehemu ngumu za meli zilizowekwa maalum kwa kazi hiyo.
|