Gharama za kwenda Hijja
zapanda Tanzania
24/07/2009

USAJILI wa mahujaji kwa ajili ya safari
ya kwenda kwenye ibada ya Hijja ya mwaka huu wa 1430AH wa Kiislamu
umeanza, huku gharama za kwenda Hijja zikipanda kidogo ikilinganishwa na
mwaka jana.
Gharama za safari ya Hijja kwa mwaka
jana ilikuwa ni dola za Marekani 3,150 lakini mwaka huu imepanda kidogo
na kufikia dola 3,200 za Marekani.
Hiyo ni kwa mujibu wa viwango vya
gharama vya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), lakini katika
taasisi nyingine gharama imepanda zaidi ya dola 3,200 za Marekani.
Akizungumza na waandishi wa habari
ofisini kwake Bakwata Makao Makuu, afisa wa idara ya Hijja, Muhidin
Hassan alisema, mahujaji wanatarajiwa kuondoka nchini kuelekea Makka,
Saudi Arabia, “Hatujajua tarehe rasmi ya kuondoka kwa Mahujaji, lakini
wataondoka ndani ya Novemba na kurudi nchini Disemba mwaka huu,” alisema
na kuongeza, “Usajili umeanza na maandalizi yanaendelea vizuri kwa
sababu watu wanajitokeza kupitia akaunti zetu kutanguliza gharama zao na
ni matumaini yetu ukifika mwezi Oktoba tutakuwa na Mahujaji wengi
waliokamilisha gharama zao.”
Alisema, gharama ya kila kichwa itakuwa
ni dola 3,200 za Marekani ambayo itatumika kwa ajili ya usafiri wake wa
ndege kwenda na kurudi Makka, na malazi katika nyumba zilizopo karibu
kabisa na misikiti mitukufu ya Makka na Madina.
“Pia fedha hizo zitatumika kwa chakula
kwa siku zote atakazokaa nchini Saudi Arabia, Matibabu na kuchinja siku
ya Idd na mavazi maalumu ya Hijja (Ihraam),” alisema Hassan na kuongeza.
“Pia fedha hizo hizo zitatumika kwa
ajili ya ziara katika maeneo matakatifu ya Makka na Madina, usafiri wa
ndani nchini Saudia na mahema katika sehemu zote atakazokaa.”
Aidha, aliwataka Waislamu wote nchini
walioweka nia ya kwenda kutekeleza ibada hiyo kwa mwaka huu, kujisajili
mapema katika ofisi za Bakwata makao makuu na matawi yake nchini kote
ili kuweza kuratibu safari hiyo mapema.
“Wakijisajili mapema itatusaidia kujua
idadi na kiasi cha mahitaji kwa Mahujaji wetu kwa siku zote watakazokaa
Makka na Madina - kwa ajili ya ibada ya Hijja,” alisisitiza.
Ibada ya Hijja inafanyika katika mwezi
wa 12 (Dhulhijja) kwa mwaka wa Kiislamu na ni mara moja tu kwa kila
mwaka, na kila Muislamu mwenye uwezo analazimika kufanya ibada hiyo
angalau mara moja katika maisha yake.
|