Mount Kilimanjaro

Beit El Ajaib
     

HomeNewsServicesEventsAbout UsContact Us

 
ProfileToolsGamesCommunity

NEWS

 
 

Ikulu yavunja ukimya juu ya madai ya Richmond

03/08/2009

SIKU chache baada ya baadhi ya wanasiasa kumhusisha Rais Jakaya Kikwete na kashfa ya utoaji wa zabuni kwa kampuni tata ya Richmond Development LLC, Ikulu imetoa msimamo wa kumtetea huku ikitaja mambo manne ambayo alihusika nayo.

Msimamo huo wa Ikulu ulitolewa jana na Katibu Mkuu Kiongozi, Phillemon Luhanjo kwenye mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, jana, akisisitiza Rais Kikwete hakuhusika kwa namna yoyote ile ya kufanikisha zabuni hiyo kutolewa kwa kampuni hiyo tata.

"Katika siku za karibuni kumekuwepo na maneno na vijembe ati kuwa, kuna mkono wa Rais Jakaya Kikwete katika kutoa tenda (zabuni) ya kuzalisha umeme wa dharura iliyopata Kampuni ya Richmond," alisema Luhanjo akisisitiza:

"Tunapenda kusema tena kwa msisitizo kuwa maneno hayo si ya kweli na hayana msingi wowote. Rais hajahusika na uamuzi wa tenda hiyo kupewa Richmond kama vile ambavyo hakuhusika na kupewa tenda kwa Kampuni za Aggreko na Alstom."

Luhanjo alitaja mambo manne ambayo Rais Kikwete alihusika katika suala zima la ukodishaji wa mitambo ya kuzalisha umeme ikiwemo ya Richmond: Kwanza, katika kuamua Tanesco itumie mitambo ya kukodi kuzalisha umeme na serikali igharamie ukodishaji huo.

Suala hilo lilikuwa lazima liamuliwe na yeye kwa sababu lilikuwa linahitaji serikali kugharamia ukodishaji. Kama si hivyo lisingefikishwa kwake kwani ni jambo ambalo lingekuwa juu ya Tanesco kuamua kukodisha na kulipia. Gharama hizo hazikuwa zimepangwa katika bajeti ya serikali, hivyo ilikuwa ni lazima kupata idhini ya rais ya kutafuta hizo pesa na kuzitumia kwa ajili hiyo.

Pili, Rais alihusika katika kuzungumza na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), kuwaomba wakubali sehemu ya pesa waliyopanga kuipa Tanzania kama msaada kutokana na mpango wa msamaha wa madeni itumike kugharamia ukodishaji wa mitambo ya kuzalisha umeme.

Walikubali, na USD 225 milioni zilitumika kukodisha mitambo ya Kampuni za Aggreko, Alstom na Richmond (ambayo baadaye ikawa Dowans) na matumizi mengine ya dharura za umeme. Matumizi hayo mengine yalijumuisha pia ununuzi wa mitambo ya aina ya Watsilla ya kuzalisha megawati 100 za umeme pale Ubungo kwa kutumia gesi asilia. Mitambo hiyo imeshanunuliwa, kufungwa na tayari inazalisha umeme.

Tatu, Rais alihusika katika vikao vya Baraza la Mawaziri vilivyojadili matatizo ya upungufu mkubwa wa umeme nchini na kuamua hatua mbalimbali zichukuliwe kukabiliana na tatizo hilo. Moja ya hatua zilizoamuliwa kuchukuliwa, ni hii ya kukodisha mitambo ya kuzalisha umeme. Katika vikao hivyo vya Baraza la Mawaziri alitoa maelekezo ya mambo ya kuzingatiwa katika zoezi zima la kupata makampuni au watu watakaotoa huduma hiyo. Hususan, rais alisisitiza kuwa pamoja na udharura uliokuwepo Kanuni na Sheria ya Ununuzi wa Umma zizingatiwe.

Nne, Rais alikataa Kampuni ya Richmond isipewe malipo ya awali (down payment) ya USD 10 milioni na kutaka ukweli kuhusu uaminifu na ukamilifu (integrity) wa kampuni hiyo ujulikane. Rais alikataa maombi yaliyopelekwa kwake na Wizara ya Nishati na Madini ya kumwomba aagize Wizara ya Fedha, iilipe kampuni hiyo fedha hizo.

Rais aliagiza Wizara ya Fedha ibaki na msimamo wake na kuitaka Wizara ya Nishati na Madini pamoja na Tanesco wafanye mambo mawili. Kwanza, wafanye utafiti zaidi kujua undani wa Kampuni ya Richmond.

Isije kuwa ni kampuni bandia wakapewa fedha wakatokomea nazo na mitambo isipatikane na hakuna namna ya kuipata kampuni wala wahusika wake. Pili aliagiza wawatake viongozi wa Kampuni ya Richmond kwanza walete mitambo, ikishafika, ndipo walipwe. Maagizo hayo ya rais yalizingatiwa na Kampuni ya Richmond ikapewa sharti hilo. Lakini, ikashindwa kulitekeleza na kuishia kuingia mkataba na Kampuni ya Dowans iliyokuja kuleta hiyo mitambo badala yake.

Hivyo ndivyo alivyohusika rais katika suala zima la ukodishaji wa mitambo ya kuzalisha umeme kutoka kwa makampuni ya Aggreko, Alstom na Richmond. Kama kweli kungekuwa na mkono wake wa upendeleo kwa Kampuni ya Richmond kupata tenda, iweje tena yeye ndiye akatae kampuni hiyo isilipwe fedha za kianzio mpaka kuifanya ishindwe kazi? alisema bwana Luhanjo.

 

   
 

Custom Search

Go up

 

Quick Links

Watch Television
News Archive

© www.zenjydar.co.uk - Since 2007 | Web master | Site map | www.zenjydar.co.uk - Since 2007 ©