Sh. Bilioni 230 msaada
kutoka Uingereza
05/08/2009

Uingereza imeipatia Tanzania Sh.
bilioni 230 kwa ajili ya kusaidia bajeti ya mwaka huu, huku ikiitaka
ijidhatiti kupambana na rushwa.
Mkuu wa
Shirika la Maendeleo ya Kimataifa ya Uingereza (DFID), Darren Welch,
aliyasema hayo alipokutana na Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo,
jijini Dar es Salaam.
Uingereza
ndiye mshirika wa maendeleo iliyotoa fedha nyingi kulinganisha na nchi
zingine. Jumla ya fedha zote zilizokwishatolewa na washirika wa
maendeleo zinafikia Sh. bilioni 424.
Welch
alisema Uingereza inatekeleza ahadi zake na imejikita kuisaidia Tanzania
hata katika kipindi hiki kigumu cha mtikisiko wa fedha duniani. Alisema
fedha hizo zimeingizwa kwenye bajeti ya serikali kwa mkupuo mmoja
mwanzoni mwa mwaka huu wa fedha kulingana na mchakato wa bajeti ya
serikali.
"Tunataka
kuona watu wengi zaidi wakipata maji safi na salama, wanawake wengi
zaidi wakijifungua salama na watoto wengi wakienda shule... Kwa hiyo
tuko mstari wa mbele kuisaidia Tanzania katika harakati zake za
kupunguza umaskini na kuboresha maisha ya watu wake," alisema. Alisema
lazima serikali ijitahidi kuboresha mazingira ya biashara ili sekta hiyo
ikue na na kuongeza ajira kwa wananchi.
Welch pia
alitangaza kuzinduliwa kwa mkakati mpya wa serikali ya Uingereza
unaohusu maendeleo ya kimataifa.
"Mkakati huu
unasisitiza nia ya Uingereza kuendelea kuchangia maendeleo ya kimataifa
hasa katika kipindi hiki kigumu cha msukosuko wa uchumi," alisema Welch.
Naye Waziri
Mkulo alisema hatua ya wafadhili hao kuisaidia Tanzania ni ishara ya
imani waliyo nayo kwa serikali ya Tanzania. Alisema Benki ya Dunia (WB)
na Benki ya Maendeleo Afrika (ADB), tayari ziko katika mchakato wa
kuisaidia serikali katika bajeti ya mwaka huu.
Alikiri
kuwa kuna udhaifu katika mfumo wa malipo ya fedha za serikali lakini
aliahidi kuwa serikali italifanyia kazi mfumo wa marekebisho ya
usimamizi wa fedha wa Tanzania uwe imara zaidi.
|