Serikali yaeleza chanzo
cha Ujambazi hivi sasa Tanzania
08/08/2009

SERIKALI imesema kukithiri kwa matukio ya
ujambazi nchini hivi sasa kunachangiwa na ongezeko la idadi ya watu
linalokwenda sambamba na kasi ya maendeleo nchini.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Waziri wa Mambo
ya Ndani ya Nchi Bw. Lawrence Masha (pichani juu), alisema Serikali
imejipanga kuhakikisha inakabiliana na kudhibiti uovu huo kwa gharama
yoyote.
Alisema Tanzania sasa ina wastani wa watu milioni 40 ongezeko
linalokwenda sambamba na maendeleo katika nyanja mbalimbali nchini jambo
linalochangia kuongezeka vitendo vya uhalifu.
"Katika nchi kama hii yenye wastani wa watu milioni 40 kukithiri matukio
ya ujambazi ni hali yenye kutarajiwa kadiri nchi inavyoendelea," alisema.
Alisema sababu nyingine ya kukithiri kwa matukio hayo ni Tanzania
kupakana na nchi zenye machafuko yanayohusisha matumizi ya silaha za
kivita hivyo kuna uwezekano mkubwa wa silaha hizo kuingizwa nchini kwa
magendo na kutumika katika uhalifu.
Bw. Masha alikiri kuwa Serikali haina uwezo wa kukidhi vitendea kazi vya
kudhibiti uhalifu hali inasababisha kutegemea misaada kutoka kwa
wahisani mbalimbali.
Alisema Jeshi la Polisi litaongeza nguvu zake kwa kujenga ukaribu na
raia na kuongeza idadi ya vituo kwa lengo la kuimarisha ulinzi
shirikishi.
Alisema wizara yake imejipanga kuwasaka wahalifu wa ndani na nje ya nchi
ili kuhakikisha amani na utulivu vinadumishwa nchini.
"Tumejipanga kusaka wahalifu Wakitanzania na wakigeni ili kuimarisha
amani nchini kwani pande zote mbili zinaweza kuwa chanzo cha uhalifu
hivyo hatuwezi kupuuzia upande mmoja, alisema Bw. Masha.
Alitoa mwito kwa wananchi kutoa taarifa zitakazosaidia kudhibiti na
kukamatwa wahalifu katika matukio mbalimbali.
|