Serikali haina mpango wa
kuongeza bei ya umeme
14/08/2009

SERIKALI imesema hakuna mpango wa
kupandisha bei ya umeme nchini kwa sasa. Akizungumza jijini Dar es
Salaam juzi, Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja alisema hakuna
kampuni wala shirika lolote nchini, linaloweza kupandisha bei ya umeme
bila kupata kibali cha serikali.
Hivi karibuni pamoja na kuwepo kwa
sheria inayoruhusu kampuni mbalimbali binafsi pamoja na Shirika la Umeme
nchini (Tanesco ) kutoa huduma ya umeme, lakini hazitakuwa na uwezo wa
kupandisha bei bila idhini ya serikali.
“Hata Tanesco walitaka kupandisha bei
ya umeme, lakini walizuiliwa na EWURA kwa kuwa wao ndio wasimamizi wa
masuala hayo na ni chombo cha serikali,” alisema.
Ngeleja ambaye alikuwa akifungua
mkutano wa Ushirikiano wa Miundombinu kwa ajili ya Maendeleo ya Afrika,
(iPAD), alisema serikali inafanya kila jitihada kuhakikisha kuwa mlaji
anapata umeme kwa bei nafuu, lakini akakumbusha wananchi kuwa umeme huo
ni lazima ulipiwe ili kuweza kuusambaza zaidi nchini.
|