Wanafunzi wateketea na
moto Iringa
23/08/2009

WANAFUNZI 12 wa kike katika Shule ya
Sekondari ya Idodi, wilayani Iringa, wamekufa kwa kuteketea kwa moto na
wengine 23 wamejeruhiwa vibaya katika tukio hilo lililotokea kipindi cha
usiku.
Habari za awali zilisema kufa na
kujeruhiwa kwa wanafunzi hao, kumetokana na moto ulioteketeza bweni lao,
saa 8 (nane) usiku wakati wakiwa wamelala.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa,
Evarist Mangalla, aliwataja waliokufa katika tukio hilo la kusikitisha
kuwa ni, Matilda Mtewele wa kidato cha kwanza, kutoka Tungamalenga,
Digna Ndunguru wa kidato cha pili,
kutoka Songea na Cheka Kuyaa, wa kidato cha pili, kutoka Makifu,
wilayani Iringa.
Wengine ni, Cesiliana John wa kidato
cha pili, kutoka Kitisi, Iringa, Lazia
Kihwele wa kidato cha pili,
kutoka Mahuninga,Witnes Mbilinyi wa kidato cha pili, kutoka mjini Iringa,
Stela
Mwigavila wa kidato cha pili, kutoka Makifu na Salha Abdula wa kidato
cha tatu kutoka Dar es
Salaam.
Marehemu wengine wametajwa kuwa ni,
Jesca Wissa wa kidato cha tatu kutoka Idodi, Maria Ndole wa kidato cha
nne kutoka Makifu, Adelphina Kwama wa kidato cha kwanza kutoka Makifu na
Elizabeth Mtavila wa kidato cha kwanza kutoka Mapogolo.
Kamanda Mangalla alisema chanzo cha
moto huo ni mshumaa uliokuwa ukitumiwa na
mwanafunzi, Naomi Mnyali,
ambaye alisahau kuuzima, baada ya kumaliza kusoma usiku huo.
Akizungumza na mwandishi wa Mwananchi,
Mkuu wa shule hiyo, Raymond Mlasu, alisema bweni lililoteketea kwa moto,
lilikuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi 461 na kwamba lilikuwa na vyumba
25.
Msalu alisema shule hiyo ina jenereta linalotumika kutoa huduma kati
ya 12 jioni hadi saa 5 usiku.
Alisema walipozima jenereta kabla ya
tukio hilo, mwanafunzi huyo aliwasha mshumaa ili kujisomea,
lakini
alipopatwa na usingizi, alisahau kuuzima, jambo lililosababisha moto
ulioteketeza bweni na hatimaye vifo vya wanafunzi.
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa wa
Iringa, Oscar Gabone,
alisema hospitali hiyo imepokea majeruhi 14 na
wengine tisa wamelazwa katika Kituo cha Afya cha Idodi.
Gabone aliwataja majeruhi waliolazwa
katika Hospitali ya Mkoa wa Iringa kuwa ni, Anoda Pambamaji, Lucy Sawani,
Evamary Calus, Anna Mlowoka, Glad Mponzi, Lela Mkuya, Mwinzarubi Elias,
Helena
Mapunda, Irene Mponzi, na Pisca Malele.
Wengine ni, Faraja Sodike, Helena
Barugu,
Upendo Nyamaduke, Veronica Nyamla na Sabrina Abdurahaman.
Kwa mujibu wa Dk Gabone, majeruhi
waliolazwa katika Kituo cha Afya cha Idodi
ni, Esta Zayumba, Lucy
Luvanda , Faraja Palino na Ares Ndaga.
Wanafunzi Sabrina na Irene walisema
vifo vya wanafunzi wenzao vimechangia na bweni hilo kuwa na mlango mmoja
wa kutokea.
Walidai kuwa katika hatua za awali za
moto huo, walinusa harufu ya
petroli na kwamba walipojaribu kutoka nje,
walisukumwa na mtu
asiyefahamika, lakini kutoka nje ya jengo.
Walisema hawakuweza kutambua jinsia
wala sura ya mtu huyo ingawa alivaa sweta lenye kofia. Kamanda Mangalla
alisema polisi na Idara ya Zimamoto, zinaendelea na uchunguzi kuhusu
kiini cha moto huo.
Janga hilo limewacha zaidi ya watoto
400 wakiwa hawana malazi, ambapo Mkurugenzi wa Kiwanda cha Maziwa cha
Assas, Salim Abri alijitolea kutoa magodoro 200 na mablangeti 200 kuweza
kuwasitiri wanafunzi hao.
"Ni kweli nimetoa vifaa hivyo baada ya
kusikia zaidi ya watoto 400 hawana malazi," alisema Salim Abri bila
kufafanua.
Kutoka Moshi, Daniel Mjema anaripoti
kuwa serikali imeahidi kugharamia mazishi ya wanafunzi hao.
Kwa mujibu wa Mjema, ahadi hiyo
ilitolewa jana na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Jumanne
Maghembe alipokuwa akizungumza na Mwananchi, mjini Moshi.
Waziri hiyo alisema pamoja na
kugharamia maziko ya wanafunzi hao, serikali pia itafanya kila
linalowezekana kuwatumia madaktari bingwa kuokoa maisha ya wanafunzi
wengine 13 waliojeruhiwa vibaya na moto huo.
"Ni tukio la kusikitisha sana,naishiwa
maneno ya kusema, lakini tukio hili ni baya sana tumepoteza vijana wetu
wapendwa pale, lakini pia tuna vijana 15 wameungua vibaya sana tuwaombee
wapone haraka"alisema Profesa Maghembe.
Profesa Maghembe alisema siku zote kifo
kinasababisha masikitiko na majonzi mengi katika familia, jamii, binafsi
na kwamba serikali inaungana na familia ya vijana hao katika msiba huu
mkubwa.
Profesa Maghembe alisema tukio hilo
limewarejeshea Watanzania huzuni na kuwakumbusha tukio lingine baya la
moto ulioua wanafunzi wa kike 43 katika Shule ya Sekondari ya
Shauritanga, mwaka 1994.
Kiini cha tukio hilo la Shauritanga
mkoani Kilimanjaro, bado hakijatangazwa hata baada ya kikosi cha
wataalamu wa uchunguzi cha Scotland Yard kilichoshirikiana na wataalamu
wa ndani.
Profesa Maghembe alisema wiki
iliyomalizika jana imekuwa ni mbaya sana kwa wizara yake kutokana na
matukio mbalimbali ya kuhuzunisha likiwamo la kuuawa kwa mwanafunzi wa
sekondari ya Umbwe, mkoani Kilimanjaro.
Exuper Kachenje anaripoti kuwa Waziri
Mkuu Mizengo Pinda, ametoa salamu za rambirambi kufuatia vifo vya
wanafunzi hao wa Shule ya Sekondari ya Idodi. Hali kadhalika, ametoa
pole kwa majeruhi wa ajali hiyo mbaya.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya
habari jana, waziri mkuu, alisema kwa niaba ya serikali na yeye binafsi,
amesikitishwa na kuhuzunishwa na tukio hilo na kuwaomba wazazi, ndugu,
jamaa na marafiki wa marehemu, kuwa na subira na uvumilivu katika
kipindi kigumu cha majonzi.
"Kwa niaba ya serikali na mimi binafsi,
natoa salamu za rambirambi kwa vifo vya wanafunzi, vilivyotokana na
ajali hiyo, nimesikitishwa na kuhuzunishwa sana na tukio hilo, nawaomba
wazazi, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu, kuwa wavumilivu na wavute
subira katika kipindi kigumu cha majonzi," alisema Pinda katika taarifa
yake.
|