Benki Kuu ya Tanzania (BoT)
kuchapisha noti mpya
16/10/2009

SERIKALI imeanza mchakato wa kuchapisha
upya fedha zake za noti zitakazokuwa na sura na muundo mpya, ambazo
zitaanza kutumika baada ya miezi minane ijayo ambapo fedha zilizopo
zitaendelea kutumika kama kawaida.
Akizungumza na waandishi wa habari jana
katika ofisi ndogo za Bunge jijini Dar es Salaam, Gavana wa Benki Kuu,
Profesa Benno Ndullu alisema tayari mchakato wa kuzipata kampuni
zitakazochapisha fedha hizo umekamilika.
"Tayari tumekwishapata kampuni mbili za
kutoka nchi mbili tofauti kwa ajili ya kuchapisha fedha zetu mpya za
noti yaani Sh 500, 1000, 2000, 5000 na 10000," alisema Profesa Ndullu.
Profesa Ndullu alifafanua kuwa serikali
imeamua kuchapisha fedha hizo ikiwa ni sehemu ya mpango wa kupambana na
uingizwaji wa fedha bandia na haramu katika matumizi, pamoja na
kuziboresha kulingana na matumizi.
Gavana huyo alisema awali kampuni 10
ziliomba tenda ya kuzichapa noti hizo, lakini ni kampuni tisa ndizo
zilizobainika kuwa na uwezo wa kuchapa fedha hizo katika kiwango
kinachohitajika.
"Tulizichuja hizo kampuni tisa na
tukapata kampuni mbili ambazo ni Cren Currency ya nchini Sweden
itakayochapisha noti za Sh 500, 2000, 5000 na 10,000, wakati noti za Sh
1000 zitachapwa na kampuni ya De-rarue ya nchini Uingereza," alisema
gavana huyo.
Profesa Ndullu ambaye hivi karibuni
alitunukiwa nishani ya gavana bora alisema kutokana na kampuni nyingi
kujitokeza kuomba tenda hiyo zimesaidia kupunguza gharama za uchapishaji
wa fedha hizo.
Katika hatua nyingne, Profesa Ndullu
alisema kimsingi hakuna sababu ya kuundwa kwa chombo maalumu
kitakachosimamia Benki Kuu katika utendaji wake.
Alisema kinachohitajika kwa sasa ndani
ya BoT ni ufanyaji kazi kwa uwazi na uwajibikaji.
Pia Profesa Ndullu alisema BoT
wanatakiwa kuwa wawazi katika ripoti zao ambazo zitasaidia ukaguzi kuwa
mzuri.
"Kinachohitaji kwa sasa ndani ya BoT ni
wafanye shughuli zao kwa uwazi na uwajibikaji na pia wawe wazi katika
ripoti zao, ili kufanya ukaguzi kuwa mzuri," alisema Profesa Ndullu.
Akizungumza hivi karibuni katika
mkutano unaohusu usimamizi na uratibu wa sekta ya kibenki nchini,
ulioitishwa na ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu nchini (CAG),
Eva Lindstr÷m ambaye ni Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
wa Sweden, alishauri kiundwe chombo kitakachosimamia Benki Kuu (BoT)
katika utendaji wake.
Lindstr÷m alisema Serikali ya Sweden
imeunda chombo hicho ambacho ni huru na kuwa siyo sehemu ya Benki Kuu.
Alisema chombo hicho ni taasisi huru ya
serikali ambayo siyo sehemu ya Benki Kuu ya Sweden, inasimamia mfumo
mzima wa kifedha nchini humo ikiwemo mabenki, mashirika ya umma na ya
mashirika ya pensheni.
Kauli hiyo ya Lindstr÷m, iliungwa
mkono na CAG, Ludovick Utouh, Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi, Omar Mzee
pamoja na mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa,
Dk Willibrod Slaa, ambao walisema kuundwa kwa taasisi hiyo huru
kutasaidia kupunguza upotevu wa fedha katika benki hiyo.
|