Waziri Aisha ataka orodha
ya mabosi waombao ngono kwa kutoa ajira
01/11/2009

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ)
imewataka wanawake wenye kuombwa ngono ya mapenzi wakati wanapotafuta
ajira sehemu za kazi watumie simu zao za mkononi kuwarekodi watu wenye
tabia hiyo ili kupata ushahidi wa madai hayo.
Waziri wa Kazi, Maendeleo ya Vijana,
Wanawake na Watoto, Asha Abdallah Juma aliwaambia wajumbe wa baraza la
wawakilishi jana wakati  akijibu maswali mbalimbali katika kikao cha
baraza la wawakilishi kinachoendelea Maisara Mjini Unguja.
Wanaodaiwa ngono ya mapenzi waseme na
wasikae kimya na siku hizi mambo yameendelea, wanazo simu za mkononi,
tunawaambia wanawake wenye simu watege sauti wanapotakiwa kimapenzi ni
kunasa sauti za watu wenye tabia hiyo angalau mtu aje na ushahidi wa
anayoyasema alisema Waziri huyo.
Alisema wizara yake inaendelea na
usimamizi wa sheria ambapo ina jukumu kubwa ya kusuluhisha migogoro hiyo
ya wafanyakazi kwa kuwarejesha kazini wale wote ambao wamefukuzwa
kinyume cha sheria au kupatiwa maslahi yao ya kazi.
Wizara kwa nyakati tofauti inawaita
ofisini mameneja na maafisa wanaotuhumiwa kuwalazimisha kingono
wafanyakazi hao, inawaonya, baadhi yao wamechukuliwa hatua za kinidhamu
na waajiri wao baada ya hatua yetu ikiwemo kuonywa vikali wengine
kufukuzwa kazi na wengine kuondoshwa nchini alisema Waziri huyo.
Waziri huyo alisema katika matatizo
yote hayo ya kufukuzwa kazi kwa wafanyakazi wa mahoteli hakuna
malalamiko yanayotokana na mahusiano ya kimapenzi.
Malalamiko hayo yote yameshughulikiwa
na Wizara yangu na wadai 29 wamelipwa haki zao ikiwemo dai moja ambapo
mfanyakazi alirejeshwa kazini. Madai na malalamiko 10 yanaendelea
kushughulikiwa alisema Waziri Asha.
Awali akijibu swali la msingi
aliloulizwa na Mwakilishi wa Jimbo la Amani (CCM) Ali Denge Makame
aliyetaka kujua kama wizara inafahamu tatizo la wafanyakazi kufukuzwa
kazini bila ya utaratibu na baadhi yao kutakiwa kimapenzi na mabosi wao.
Waziri Asha alisema serikali inafahamu
suala hilo na ndio maana inachukua hatua madhubuti ili kuweza
kukabiliana na tatizo hilo ikiwa pamoja na kushughulikia malalamiko ya
wafanyakazi wanaofukuzwa kazi bila ya kufuata utaratibu wa kazi kama
unavyoelekeza.
Alisema kumekuwepo na manung'uniko na
malalamiko ambayo baadhi yake yamewasilishwa wizarani kutoka kwa baadhi
ya waafanyakazi wa mahoteli kwamba wanafukuzwa kazi na waajiri wao bila
ya taratibu za kisheria kufuatwa.
Alisema katika kipindi cha januari hadi
octoba mwaka huu wizara ya hiyo imepokea jumla ya madai na malalamiko 39
ya kufukuzwa kazi kwa Unguja na Pemba ambapo hakuna madai ya maandishi
yaliowasilishwa yanayohusu kulazimishwa kingono na mabosi wao.
|