Hospitali ya Muhimbili
yafanyiwa ukarabati
04/11/2009

HOSPITALI ya Taifa Muhimbili inafanyiwa
mabadiliko makubwa pamoja na jengo la Chuo kikuu cha Muhimbili. Rais
Jakaya Kikwete amewataka Watanzania kutoenda kutibiwa katika hospitali
ya Taifa Muhimbili wakitokea majumbani mwao bali waende baada ya kupata
rufaa za hospitali za wilaya na rufaa. Rais alitoa kauli hiyo wakati wa
ziara yake iliyoambatana na ufunguzi wa kitengo cha matibabu ya Figo.
“Muhimbili
inapaswa kuwa ni hospitali ya kutibu magonjwa makubwa yanayoweza
kupelekwa nje ya nchi, lakini magonjwa ya kawaida yanapaswa kutibiwa
katika hospitali ya Wilaya pamoja na Zahanati”, alisema Rais Kikwete na
kuongeza, “Hii ni hospitali ya rufaa inayopokea wagonjwa kutoka
hospitali zingine si kila mgonjwa anapaswa kutibiwa hapa wengine
watibiwe kwenye hospitali zilizoko jirani na maeneo wanakoishi wagonjwa”.
Rais pia lisema kuwa lengo la serikali ni kuwapatia wananchi huduma bora
ya afya na ndiyo maana hivi sasa kuna sera ya kujenga vituo vya afya na
zahanati jirani na makazi ya wananchi. Kuhusu hatua ya Watanzania kwenda
kutafuta matibabu ya nje ya nchi Rais Kikwete alisema serikali
inaendelea kufanya jitihada za kuboresha huduma ya afya nchini ili
wananchi wasiende kutibiwa nje ya nchi.

“Hakuna haja ya Watanzania kwenda
kutibiwa nje ya nchi kwa sababu hivi sasa tunajitahidi kuboresha huduma
ya afya nchini kadri ya uwezo wetu katika hospitali hii ya muhimbili”.
Alisema Rais, “Nimeelezwa kuwa hivi sasa kuna kitengo cha matibabu ya
Figo hapa Muhimbili hivyo watu wanaohitaji kubadilisha damu watapata
huduma hiyo hapa hakuna haja ya kwenda Kenya au India kwa ajili ya
kubadilisha damu” alifafanua Rais Kikwete. Aliongeza kuwa “Hapo nje
tumeonyeshwa ramani ya majengo mawili makubwa yanayojengwa na Wachina
yatakapo kamilika yatatumika kwa ajili ya upasuaji wa moyo”.
Mbali na ufunguzi wa kitengo hicho cha Figo, Rais pia alifungua jengo
jipya la kitengo cha matibabu ya dharura iliyofunguliwa na taasisi ya
misaada ya Kibinadam ya ‘Abbott Fund’.
|