Serikali ya Libya kusaidia
walioathirika Kilosa
17/01/2010

Jamhuri
ya watu wa Libya imetoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa wahanga wa
mafuriko ya Kilosa mkoani Morogoro, ikiwa ni pamoja na kuwajengea nyumba
200 zenye thamani ya shilingi bilioni 1.5.
Akiongea na wanahabari katika uwanja wa ndege Dar es Salaam Waziri wa
nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Uratibu na Bunge) Mheshimiwa Philip
Marmo alisema msaada huo umekuja wakati muafaka, kwani hali ya wahanga
hao si ya kuridhisha.
Aidha Waziri Marmo alizitaka nchi rafiki, Jumuiya za Kimataifa pamoja na
Watanzania kwa ujumla kutoa misaada kwa hiari yao kwa kadri wanavyoguswa
kwa wahanga wa mafuriko ya Kilosa.
“Uwezo wa Serikali ni mdogo na hauwezi kutosheleza kila kitu hivyo
tunaomba Jumuiya mabalimbali za Kimataifa na Watanzania Kushirikiana
katika kutoa misaada”. Alisema.
Pia alizitaka Kamati za maafa husika kutekeleza wajibu wao kwa kufikisha
misaada hiyo kwa wahusika na alimhakikishia balozi wa Libya nchini,
bwana Ahmed Abdulsalaam Al Ashaab, ambaye alikabidhi msaada huo kwa
niaba ya nchi yake kuwa itawafikia walengwa na magari yataanza kupeleka
misaada hiyo kesho.
Akikabidhi msaada huo balozi wa Libya nchini bwana Ahmed Abdulsalaam Al
Ashaab alisema msaada huo umetolewa na jumuiya mbalimbali nchini humo
kutokana na ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na Libya.
Vifaa vilivyotolewa ni Magodoro 1100, Blanketi 400, Mahema 1300, Mito
1200, Maboksi 500 ya madawa ikiwa ni pamoja na vifaa vya huduma ya
kwanza.
|