Mount Kilimanjaro

Beit El Ajaib
     

HomeNewsServicesEventsAbout UsContact Us

 
ProfileToolsGamesCommunity

NEWS

 
 

Balozi Mwanaidi atetea haki za Wafanyakazi wa ndani ughaibuni

22/02/2010

Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mheshimiwa Mwanaidi Maajar, amependekeza kukazwa sheria za kuwalinda wafanyakazi wa ndani wanaosafirishwa kufanya kazi za utumishi nchi za kigeni.

Akiongea nami jana Jumapili mjini London, Mama Maajar alikuwa akitoa maoni kuhusu kukamatwa na kuchunguzwa na polisi kwa baadhi ya waajiri wa Kitanzania hapa Uingereza wanaowaleta wafanyakazi wa ndani na kutotimiza ahadi walizowapa kabla ya safari.

“Tunachokiona ni kuvunjwa kwa makubaliano ya kuaminiana kati ya wafanyakazi na waajiriwa,” alisisitiza.

Mwezi Desemba mwaka jana maofisa wawili wa polisi wa Kiingereza walisafiri Bongo kwa majuma mawili kama sehemu ya uchunguzi wa mateso aliyofanyiwa Bi. Zubeda Ali na waajiri wake, mjini Birmingham toka 2007.

Waajiri hao, Bwana na Bibi Shariff, ambao wamewekewa dhamana hadi kesi yao itakapofikishwa tena mahakamani mwezi ujao walitiwa hatiani mwezi jana kwa mashtaka ya kusafirisha wanadamu kinyume cha matakwa yao na kukiuka masharti ya uhamiaji.

Mwishoni mwa wiki jana mwajiri wa mfanyakazi mwingine wa makamo mzawa wa Kondoa alihojiwa na polisi wa London baada ya mfanyakazi huyo kupelekwa hospitali akiwa na ugonjwa wa kuvimba miguu (Varicose Veins).

Bibiye alifanya kazi kutwa kucha bila mapumziko wala likizo na kulala jikoni. Mshahara wake mdogo (shilingi elfu 20) alipewa mwisho wa mwaka si kwa mwezi. Mwajiri wake alimwita kwa kengele kama mbwa badala ya kutumia jina lake. Kwa sasa anahifadhiwa na kutetewa na chama kinachopigania maslahi ya wafanyakazi wa ndani (Kalaayan) na Umoja wa Wanawake wa Tanzania London (TAWA).

Balozi Maajar kasema wafanyakazi hawa wa ndani hudanganywa kwamba watalipwa vizuri na waajiri wao. “Wakiambiwa watalipwa shilingi laki mbili ughaibuni wanaona nyingi lakini punde wanakutana na maisha tofauti na yale waliyoahidiwa.”

Mheshimiwa Maajar alisema Ubalozi wa Tanzania umekuwa ukishirikiana na taasisi mbalimbali husika hapa, polisi wa Uingereza na TAWA kuwasaidia wanawake hawa.

Ila alisema tatizo hili halipo UIngereza tu. “Karibuni nimesoma habari mtandaoni kuhusu unyanyasaji wanaofanyiwa wafanyakazi wa Kibongo nchi za Uarabuni.”

Aliendelea kueleza kuwa wengi wa waajiri hawa ni watu wanaoheshimiwa Bongo na hawakubali kwamba wanachokifanya si kizuri. Wamezoea kuwafanya binadamu wenzao watumwa.

“Iko haja ya kuwafichua maana majina yao yameshawekwa hadharani hapa na kesi ziko mahakamani. Je, watajisikiaje kama hawa wanawake wangekuwa binti zao?”.

Habari na Freddy Masha.

 

   
 

Custom Search

Go up

 

Quick Links

Watch Television
News Archive

© www.zenjydar.co.uk - Since 2007 | Web master | Site map | www.zenjydar.co.uk - Since 2007 ©