Hati ya Nyumba
10/05/2010

Katika historia tunajifunza kwamba katika
jamii mbalimbali ardhi ndiyo ilikuwa njia kuu ya uchumi, lakini pamoja
na sifa zote hizo ilizonazo, ardhi inaweza kukunufaisha kama utajua
kuitumia kwa kadri sheria inavyoruhusu.
Kimsingi kwa mujibu wa sheria, ardhi
inamilikiwa na serikali na wananchi wake hupewa umiliki wa muda tu kwa
mujibu wa sheria kuanzia miaka 33 hadi 99 kutegemea na maombi na
matumizi yaliyokusudiwa na mwombaji.
Ili kupata uhalali wa umiliki wa ardhi,
mwombaji anaweza kutambulika kama mmiliki kwa kutumia sheria ya kimila
ambayo inatambua umiliki wa ardhi kwa Mtanzania ambaye itadhihirika kuwa
bila ya shaka alikuwa akiimiliki tangu kipindi cha kale na mamlaka za
eneo husika zinatambua umiliki wake huo.
Inawezekana kabisa hati ya ardhi yako
ikapotea na usijue pa kuipata tena kama zinavyoweza kupotea nyaraka
nyingine katika mazingira ambayo tumezoea kuyatambua kama ni bahati
mbaya.
Lakini pia ni kutokana na unyeti wake
katika maisha ya wanadamu, ni rahisi ardhi kufanyiwa hujuma na mtu
yeyote na mara nyingi na mtu au watu unaowaamini na wakaribu katika
maisha yako ya kila siku kuhusika na upotevo wa kiwanja chako.
Awe rafiki yako kipenzi, mwanao au hata
wakati mwingine mkeo au rafiki yako wa kike au kiume kuamua kuificha
hati ya nyumba au kuwanja chako akiamini mwisho wa siku anaweza kuuza
nyuma ya mgongo wake na kujipatia fedha kwa njia rahisi kwa sababu tu
anatumia hati halisi katika kufanya biashara hiyo.
Hii inatawaliwa na dhana potofu miongoni
mwa wananchi kwamba ukiwa na hati halisi hata ya kiwanja ambacho si
chako kimsingi ndiyo una nguvu na mamlaka ya kufanya utakacho juu ya
kiwanja au nyumba husika.
Kwa msimamo wa taratibu za kisheria kuiba
au kuficha hati ya mtu mwingine haina maana au athari yoyote katika
umiliki wake juu ya ardhi husika zaidi ya kusumbuana na kupotezeana muda
tu na wakati mwingine hata kukusababishia kuishia jela kwa tuhuma za
wizi au utapeli.
Ni vyema pindi baada ya kutambua kwamba
hati yako ya nyumba au kiwanja haionekani na huna taarifa sahihi za
kupatikana kwake kuanza kwa kutoa taarifa katika kituo cha polisi
kilicho karibu nawe na baada ya hapo utapatiwa hati maalumu ya taarifa
ya kupotelewa ambayo ndiyo itatumika kama leseni ya kutambulika kwa
maelezo yako katika ofisi za ardhi husika.
Baada ya kukamilika kwa taratibu zote hizo
za msingi ikiwa ni pamoja na kuijaza fomu maalumu za kisheria ambazo
huandaliwa na wanasheria mbalimbali ofisi ya ardhi husika hubatilisha
hati iliyopotea na kukupatia kivuli cha hati halisi ambacho kufuatia
kufikishwa na kukubalika kwa taarifa hizo katika ofisi husika ya ardhi
hati halisi iliyotolewa ndiyo huchukua nafasi ya hati halisi.
Kwa maana hiyo ndiyo kusema kwamba pindi
baada ya kuidhinishwa kwa uhalali wa kutumia hati kivuli, hati halisi
popote ilipo huwa si halali tena na yeyote ambaye ataitumia kwa namna
yoyote ile iwe kuuza au kuchukulia mkopo katika benki au taasisi yoyote
ya fedha atakuwa anakinzana na sheria ambayo haitasita kuchukua mkondo
wake dhidi yake.
Mchakato wa kutoa taarifa na kushughulikia
kupatikana kwa hati mpya unalazimika kufanyika mapema iwezekanavyo pindi
baada ya kutambua upotevu wa hati husika ili kuepuka kutoa nafasi kwa
aliyeichukua kwa nia mbaya kuweza kufanya taratibu za uhamisho kabla ya
mhusika.
Hii ni kuhimiza umuhimu wa kuangalia na
kupitia mara kwa mara hifadhi ya nyaraka majumbani kwetu ili kuepuka
kuja kushtuka wakati mwizi wako ameshafanya taratibu zote muhimu
zinazokubalika na zisizokubalika ilimradi tu kukupoka haki yako ya
umiliki wa ardhi.
Utaratibu huu utarahisisha kujiridhisha
kwako juu ya usalama wa nyaraka zako muhimu na hata kuweza kuchukua
hatua za haraka baada ya kugundua upotevu wa hati husika.
Utaratibu wote huu mpaka kupatikana kwa
hati vivuli huchukua muda mfupi na kuhusisha gharama ndogo isiyozidi
10,000 za Kitanzania bila ya kujali thamani ya ardhi au nyumba husika.
Hivyo ni vyema kwa yeyote mwenye
kupotelewa na hati kukimbia katika ofisi za ardhi mapema baada ya
kujiridhisha kuwa hati husika haipo mahala pake kama alivyokuwa
amehifadhi awali badala ya kuhangaika kutafuta mpaka mahala
kusikotafutika.
|