Kenya yawa nchi ya tano
kutia saini makubaliano ya
rasilimali ya mto Nile
21/05/2010

Kenya
imetia saini mkataba mpya wa kugawana maji ya mto Nile baada ya nchi nne
nyingine kufanya hivyo wiki iliyopita.
Ethiopia, Rwanda, Tanzania na Uganda zilitia saini mfumo huo wa
ushirikiano katika bonde la mto Nile siku ya Ijumaa licha ya upinzani
mkubwa kutoka kwa nchi za Egypt na Sudan.
Waziri
wa maji nchini Kenya Charity Ngilu amesema kuwa ni jukumu la Egypt na
Sudan sasa kuingia katika mkataba huo na kukubaliana na mataifa hayo
kugawana maji ya mto Nile.
Makubaliano hayo mapya yanachukua nafasi ya mkataba uliotiwa saini mwaka
1959 kati ya Egypt na Sudan ambao unatoa udhibiti kwao wa zaidi ya
asilimia 90 ya maji ya mto huo.
mataifa
ambayo mto huo unapitia yanataka kutekeleza miradi ya mabwawa ya umeme
na umwagiliaji kwa kushauriana na Egypt na Sudan, lakini bila ya Sudan
kuwa na kura ya turufu iliyopewa na mkataba wa enzi za ukoloni na
Uingereza mwaka 1929.
|