Safari ya Vifaru sita
kurudi Afrika yaanza
24/05/2010

Hatimaye ile safari ya kurejesha vifaru weusi 6 na wengine hadi
watakapotimia 32 kutoka nchini Afrika Kusini hadi Tanzania imeanza na
inatarajiwa kukamilika ndani ya miaka mitatu.
Hii si
mara ya kwanza kwa vifaru kurejeshwa Tanzania toka ugenini kwani mwaka
jana vifaru wengine walirejeshwa toka nchini Czech.
Vifaru hao
wanarejeshwa katika mbuga ya Wanyama ya Taifa iliyoko Serengeti baada ya
wazazi wao kuchukuliwa mwaka 1961 kutoka Tanzania ili kuwalinda dhidi ya
kutoweka kutokana na uwindaji wa kinyume na sheria. Vifaru weusi ni
mojawapo ya viumbe waliojumuishwa katika kundi la wanyama waliomo katika
hatari ya kutoweka katika uso wa dunia. Inaripotiwa kuwa nchini
Tanzania, idadi ya vifaru wa aina hiyo ni 70 tu. Ikiwa utaratibu huo
utafanikiwa kama ilivyopangwa, basi eneo la hifadhi ya wanyama pori la
Serengeti-Mara ndilo litakalokuwa na hifadhi kubwa kuliko zote duniani
la vifaru weusi.
Gharama za kuwarejesha vifaru kutoka Afrika Kusini hadi Uwanja wa Ndege
wa Kilimanjaro (KIA) kisha kusafirisha kwa barabara hadi hifadhi ya
Ngorongoro hao zinakadiriwa kuwa dola za Kimarekani laki moja
($100,000). Hifadhi ya Taifa ya Wanyamapori ya Ngorongoro tayari ina
vifaru wapatao 24 ambao wana vifaa maalumu vya ulinzi (GPS) ambavyo hurekodi nyendo
zao na mahali walipo kila wakati ili hivyo kuwalinda dhidi ya hatari na
wawindaji wa wanyama kinyume na sheria wanaosaka pembe zao ambazo huuzwa
katika masoko ya kinyume na sheria barani Asia. Uwindaji wa kinyume na
sheria umeangamiza asilimia 90% ya vifaru weusi katika kipindi cha miaka
40 (mwaka 1970 ilikadiriwa kuwepo vifaru weusi 60,000 barani Afrika).
Kutokana na ulinzi madhubuti, idadi ya vifaru hao imeendelea
kuongezekana sasainakadiriwa kuwa wapo vifaru weusi wapatao 4,200 barani
Afrika na inatarajiwa kuwa vifaru hao watakapofika Tanzania, basi idadi
yao itaendelea kuongezeka.
Usimamizi wa utaratibu mzima wa kurudishwaji viboko hao utasimamiwa kwa
ushirikiano wa Wizara ya Utalii na Maliasili ya nchini Afrika Kusini
--South African National Parks (SANParks), Shirika la Hifadhi ya Wanyama
Pori Tanzania, Tanzania National Parks (TANAPA), na Shirika la Utafiti
wa Viumbemwitu Tanzania, Tanzania Wildlife Research Institute (TAWIRI),
na shirika la Frankfurt Zoological Society (FZS) la nchini Ujerumani.
|