DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL
COMMUNICATIONS
UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
Telephone: 255-22-2114512, 2116898
E-mail:
press@ikulu.go.tz
Fax: 255-22-2113425
PRESIDENT’S OFFICE,
THE STATE HOUSE,
P.O. BOX 9120,
DAR ES SALAAM.
Tanzania.
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
KAMA ambavyo mmekuwa mnaandika na
kutangaza ni kwamba Jumanne, Juni 8, mwaka huu, 2010, magari
yanayombeba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yaliyokuwa
yametangulia kumsubiri Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete kwa
ajili ya ziara yake ya siku mbili mkoani Kilimanjaro yalishindwa
kuwaka baada ya kuwa yamewekewa mafuta kwenye Kituo cha Rafiki
kilichoko kwenye Mzunguko wa Barabara wa Arusha Road mjini Moshi.
Suala hili limezua mjadala mkubwa,
na linaelekea kupotoshwa kwa kiasi fulani na baadhi ya vyombo
vya habari. Ili kuuwezesha umma wa Watanzania kufahamu ukweli na
undani wa kilichotokea siku hiyo tunapenda kutoa ufafanuzi wa
tukio hilo kama ifuatavyo:
-
Kwamba asubuhi ya siku hiyo ya
Jumanne, wiki hii, kiasi cha saa tano asubuhi, magari matano,
aina ya Toyota Land Cruiser, ambayo ni sehemu ya magari
yanayombeba Mheshimiwa Rais, baada ya kuwa yamepitishwa
katika taratibu zote za maandalizi, yalifika kwenye Kituo
cha Rafiki kunywa mafuta ikiwa ni maandalizi ya mwisho kabla
hayajaenda kumpokea Mheshimiwa Rais kwenye Uwanja wa Ndege
wa KIA. Baada ya kujazwa mafuta, magari matatu kati ya hayo
yalikataa kuwaka, na kuona hivyo uamuzi ukachukuliwa
kutokuyawasha kabisa yale mengine mawili.
-
Kwamba Kituo hicho cha mafuta
ni moja ya vituo ambavyo vimekuwa vinatumiwa kujaza mafuta
ya magari ya Mheshimiwa Rais siku nyingi, na wala magari ya
Mheshimiwa Rais hayakwenda kujaza mafuta kwenye kituo hicho
kwa kushtukiza ama kwa bahati tu kwa sababu uamuzi wa wapi
magari ya Mheshimiwa Rais yanakunywa mafuta haufanywi na
madereva wa magari hayo.
-
Kwamba mpaka yanaingia kwenye
Kituo hicho, magari hayo yalikuwa mazima, imara na salama
kwa ajili ya kwenda kumpokea Mheshimiwa Rais ambaye alikuwa
anatokea Dar es Salaam, na kuwa tatizo lilianza baada ya
kuwa yamejazwa mafuta.
-
Kwamba pamoja na tatizo hilo,
bado msafara wa Mheshimiwa Rais ulipokelewa kama ilivyokuwa
imeandaliwa bila tatizo lolote, kwa sababu misafara ya
Mheshimiwa Rais inakuwa na mipango mbadala ya usafiri yenye
kiwango kile kile cha juu kabisa cha usalama.
-
Kwamba magari yaliyopata
tatizo la mafuta hayakutumika katika msafara huo wa ziara ya
Mheshimiwa Rais katika Mkoa wa Kilimanjaro kwa sababu
yalikuwa bado yanasafishwa. Baada ya kuwa yamesafishwa na
kuwekewa mafuta mengine yameweza kuwaka, na sasa yako njiani
kurejea Dar es Salaam.
-
Kwamba uchunguzi wa tukio zima
sasa uko mikononi mwa vyombo husika vikiwamo Jeshi la Polisi
na Mamlaka ya Usimamizi wa Nishati na Maji (EWURA).
Uchunguzi huo ukikamilika wananchi watajulishwa nini hasa
kilisababisha magari hayo kuzima baada ya kuwekewa mafuta.
Huo ndio ukweli wa tukio lile la
Jumanne mjini Moshi, na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais
inapenda kuwahakikishia wananchi yafuatayo:
-
Kwamba tukio hilo hakuliathiri
kwa namna yoyote ile ama hata kugusa usalama wa Mheshimiwa
Rais ama mipango yake ya ziara yake Mkoani Kilimanjaro.
Ziara ilikwenda na kufanyika kama ilivyopangwa, tena kwa
mafanikio makubwa sana.
-
Kwamba tukio hilo
halikusababishwa na uzembe ama kutojali kwa maofisa
waliopewa dhamana ya kusimamia shughuli za Mheshimiwa Rais.
-
Kwamba usalama wa Mheshimiwa
Rais hauna shaka yoyote, na uko mikononi mwa watu makini,
salama, watu wazalendo wanaojali usalama wa Mheshimiwa Rais
na nchi yetu, na watu wa kuaminika kabisa.
-
Kwamba tunawaomba waandishi wa
habari kutojiingiza katika ubashiri usiokuwa na msingi wala
tija katika suala hili, badala yake wasubiri ripoti kamili
ya mamlaka husika zinazochunguza tukio hili.
-
Aidha, tunawaomba wananchi
wawe na subira kuhusu tukio hilo, na kuwa watajulishwa
matokeo kamili ya nini kilisababisha hali ile pale Moshi.
Nawashukuruni sana kwa
kunisikiliza.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
10 Juni, 2010