Clinton azuru Tanzania
23/06/2010

Raisi Jakaya Kikwete amefanya mazungumzo
na Rais Mstaafu wa Marekani, Bill Clinton ambaye amekuja Tanzania
kutembelea na kuangalia shughuli zinavyoendelea katika mfuko wake
unajishughulisha na shughuli za upatikanaji wa huduma za afya duniani,
Clinton Health Access Initiative (CHAI).

Katika mazungumzo yao, pamoja na Rais
Kikwete kumshukuru Clinton kwa mchango wake hapa nchini kwa sekta ya
afya, viongozi hao walizungumzia hali ya kisiasa na maendeleo ya
Tanzania.

Mchango huo wa Clinton hapa nchini ni katika masuala ya HIV/AIDS ambapo
mfuko wa Bill Clinton unasaidia kutoa dawa za kupunguza makali na athari
za Ukimwi (ARVs).
Clinton amekuwa mstari wa mbele katika kuchangia kampuni nyingi kupewa
nafasi ya kutengeneza dawa za ARV na hivyo kuweza kushuka kwa bei na
hatimaye watu wengi hasa katika nchi masikini kuweza kumudu bei ya dawa
hizo.

Kutokana na jitihada hizo serikali imeweza kuanzisha mpango wa kitaifa
wa huduma na matibabu wa mwaka 2003 (National HIV/AIDS Care and
Treatment Plan 2003), mpango ambao umeandaliwa kwa pamoja baina ya
serikali na CHAI.
Mpango huu unalenga kuhakikisha kuwa watu waishio na virusi vya Ukimwi
wanapata huduma na dawa bila kujali hali zao za kiuchumi au uwezo.
Mfano wa Juhudi za CHAI za kuhakikisha huduma za afya zinapatikana ni
katika Mikoa ya Lindi na Mtwara ambapo waathirika wanapata huduma za
awali ikiwemo vipimo na dawa katika vituo vya maabara ya kisasa huko
huko vijijini, wilayani na Mikoani. Pamoja na dawa, CHAI pia inatoa
mafunzo kwa maafisa wa afya wanaotoa huduma.
Jana mchana Clinton alitembelea kituo cha Afya cha Kitere kilichoko
Mtwara Vijijini na kurejea jijini jioni. Clinton ataondoka nchini leo
kuelekea Afrika Kusini.
Bill Clinton alizindua rasmi mradi wa CHAI
tangu mwaka 2007
bonyeza hapa.
|