Kabla ya kuanza kwa mechi ambapo
Rais kikwete alikuwa mgeni rasmi,
baada ya kukagua timu na
kusubiri nyimbo za taifa, hakuna
kilichosikika.
Mpaka sasa bado haijafahamika
kwanini nyimbo hizo zilishindwa
kupigwa. Kufuatia kitendo hicho,
TFF imeamua kumsimamisha kazi
msemaji wa TFF, Florian Kaijage
kwa kuwa ndiye aliyekuwa amepewa
jukumu la kusimamia jambo hilo,
mpaka hapo uchunguzi
utakapokamilika.
Rais wa TFF, Leodegar Tenga
amesema kwa kushirikiana na
Wizara ya Habari Utamaduni na
michezo, wanaunda kamati itakayochunguza
chanzo cha tatizo hilo huku
Kaijage akiwa nje mpaka uchunguzi
utakapokamalika. Akaongeza
kusema kuwa tukio hilo ni la
aibu mbele ya Rais Jakaya
Kikwete, washabiki na wageni
wengine na mbaya zaidi kwa vile
mchezo huo ulionyeshwa katika
luninga ndani na nje ya nchi,
hivyo aibu hiyo imeshuhudiwa na
wapenzi wa soka kote duniani.
“Kushindwa upigaji nyimbo za
taifa ni upungufu mkubwa
kiutendaji na kama nilivyosema
hapo awali ni aibu kwa taifa
letu, napenda kwa niaba ya TFF
kuomba radhi kwa Mheshimiwa Rais,
wapenzi waliofurika uwanjani,
Watanzania kwa jumla na wageni
wetu kutoka Morocco” alisema
Tenga.
Amesema jambo hilo halikustahili
kutokea kwa kuwa liliishawahi
kutokea wakati wa mechi na
Brazil ambapo wahusika walionywa
na kupewa jukumu la kuhakikisha
wanazijaribu nyimbo zote siku
mbili kabla ya mchezo na
kuhakikisha kuwa hakuna hitilafu
yoyote na wahusika
walimuhakikishia kuwa
hakutatokea dosari yoyote.
Alisema kuanzia sasa, hata kama
mitambo ya uwanjani ni mizima,
patakuwepo bendi za Polisi/Jeshi
ama mitambo ya tahadhari kwa
ajili ya nyimbo za taifa na
matangazo mengine muhimu.
Aidha, katika hatua nyingine
Tenga amesema ndani ya mwezi
mmoja TFF inatarajia kutangaza
nafasi mbili za ajira
zilizoachwa wazi, ambazo ni ya
sasa ya Msemaji wa shirikisho
hilo na ile ya Katibu wa TFF
ambapo awali ilikuwa ajira ya
Frederick Mwakalabela ambaye
alijiengua ili kugombea Ubunge
wa Iringa Mjini (CCM).