Kampuni ya
Maegesho ya Taifa (NPS), inatarajia
kuanza kutoa huduma ya uegeshaji kwa
kutumia mfumo wa mashine maalumu
utakaosaidia kuongeza mapato na pia
kupanua huduma zake katika maeneo
mengine ya Jiji la Dar es Salaam.
Akizungumza juzi, Mkurugenzi Mtendaji wa
Kampuni hiyo, Hassan Khan, alisema
utaratibu wa kutumia mashine hizo
unatarajia kuanza rasmi Novemba 15.
Alisema, mashine hizo ambazo zitatumika
kwa mara ya kwanza nchini na Afrika,
zitaongeza kipato kwa kuwa zitadhibiti
mapato yatokanayo na uegeshaji.
Khan alisema, mashine hizo zitakuwa za
aina mbili, moja ikiwa ni ndogo
itakayokuwa ikishikwa na wahudumu
mikononi huku nyingine zikifungwa
mitaani kwa ajili ya waegeshaji
kujihudumia wenyewe.
“Kwa kuanza, hizi mashine za mitaani
zitahudumiwa na watoa huduma wetu,
kwamba mwegeshaji atamkabidhi ada ya
uegeshaji na kuitumbukiza kwenye mashine
na kumpa tiketi yake,” alisema Khan.
Alisema lengo la kufanya hivyo ni
kuondoa udanganyifu unaoweza kufanywa na
mwegeshaji.
“Unajua hata Ulaya, watu wa aina hiyo
wapo, mtu badala ya kuweka fedha halali
anatumbukiza hata fedha za aina tofauti
na zilizokusudiwa,” aliongeza Khan.
Kuhusu kupanuka kwa huduma za uegeshaji,
alisema baada ya kuanza kazi kwa huduma
hizo, watakwenda hadi pembeni mwa Jiji
na kutoza ushuru wa uegeshaji.
“Maeneo yote ambapo pia kuna utaratibu
wa kuegesha magari bila mpango tutaanza
kukusanya ushuru wa maegesho; Tegeta,
Mbezi na maeneo mengine mengi yaliyopo
pembeni mwa mji, kabla ya hapo mapato
yalikuwa yanakusanywa Kariakoo na
katikati ya Jiji,” aliongeza Khan.
Aidha, alisema wanatarajia kuongeza
idadi ya wafanyakazi hadi 1,000 kwa
ajili ya ufanisi wa kazi hiyo, ambapo
kwa sasa alisema kampuni hiyo ina
wafanyakazi 355.
Mfumo huu
pengine ni mzuri kwa kudhibiti magari na
kwa mapato, lakini la kujiuliza ni kuwa
si wananchi wote wenye uwezo wa
kulipishwa ada hizo ambao wao wenyewe
mapato yao ni madogo kwa maisha yao hasa
pembeni mwa mjini na nje kidogo ya jiji.
Na si suala la kufananishwa na Ulaya,
angalau kwa sasa.